Monday, 18 May 2015

Mulika vivutio vya Utalii Arusha

Unapatikana katikati ya Miji miwili (2) maarufu ya Cairo nchini Misri na Cape Town nchini Afrika Kusini katika umbali wa kilometa 5,233.5. Arusha hutambulika kama kitovu cha sekta ya utalii kipatikanacho Kaskazini mwa Tanzania. Mkoa wa Arusha  umejaaliwa kuwa na muonekano mzuri wa kimazingira na wingi wa viumbe hai ikiwemo wanyama na mimea tofauti na ya kuvutia, hali ya hewa iliyo bora na ya kupendeza, watu wenye haiba ya ukarimu pamoja na vivutio vingine vya utalii vikiwemo hifadhi za Taifa ka vile, Arusha, Tarangire, Manyara na Ngorongoro crater ambayo ni moja ya maajabu ya asili ya dunia na chimbuko la mwanadamu wa kale katika bonde la Olduvai ( Olduvai gorge) na pia Arusha ni lango kuu la kuingilia katika mbuga maarufu ya Serengeti. 

Katika suala la ufikikaji Jiji la Arusha ni kama “kitovu cha Utalii” na ni rahisi kufikika kwa njia ya barabara na anga pia. Kuna Barabara kuu zenye lami, mambazo huleta watu kutoka mikoa mbalimbali inayoizunguka na ile ilipatikanayo mbali. Pia unaweza kifika kwa usafiri wa anga kwa kupitia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro na Uwanja mdogo wa Ndege wa Arusha. Pamoja na hayo Arusha ni sehemu pekee yenye hoteli nyingi na nzuri pamoja na nyumba za kulala wageni ambazo zinapatikana kwa viwango tofauti zinazokidhi mahitaji na bajeti ya wageni.

AINA ZA UTALII ZIFANYIKAZO ARUSHA

Pakiwa kama kitovu cha utalii nchini Tanzania, Jiji la Arusha kulingana na maliasili zipatikazo pamoja mandhari zake tofauti tofauti za kuvutika, Arusha ni sehemu mojawapo ambayo aina mbalimbali za utalii hufanyika. Sifa hii imepelekea Jiji la Arusha kupokea wageni wengi kutoka ndani na nje ya nchi ili kuja kujionea mambo mbalimbali ya kuvutia yanayopatika katika Jiji hili. 

Aina hzo za utalii ni pamoja na:
·         Utalii wa mbuga na kuvinjari nyikani
·         Utalii wa kupanda milima
·         Utalii wa uwindaji
·         Utalii wa kitamaduni
·         Utalii wa ikolojia (Ecotourism)
·         Utalii wa malikale
·         Utalii wa mikutano
·         Utalii wa matibabu
·         Utalii wa mashambani
·         Utalii wa miji


ORODHA YA VIVUTIO VIPATIKANAVYO ARUSHA

MLIMA MERU



Kuwa na volkano isiyo hai , Milima Meru ni wa pili kwa ukubwa Tanzania ukiwa na kilele  kilicho simama katika futi 14980 ft ( 4566 m) kutoka usawa wa bahari nyuma ya Milima Kilimanjaro. Mlima Meru wenye muonekano mzuri na rahisi ukiwa katikati ya Mji wa Arusha, ni moja kati ya milima ipatakanoyo kaskazini mwa Tanzania katika moyo wa Hifadhi ya Taifa ya Arusha. Mara ya mwisho kutoa volkano yake ndogo, inasemekana ni zaidi ya karne iliyopita. Unaweza kupata muonekano mzuri na bora wa Mlima Kilimanjaro kutoka Mlima Meru, kwani ipo chini ya maili 50 kutoka Milma momja kwaenda mwingine.
Mlama Meru ni chaguo sahihi kwa wale wanaotaka kuchanganya upandaji wa Milima huku ukishuhudia baadhi wa wanyama pori wakati ukielekea kileleni mwa mlima. Wakati Milima Kilmanjaro ukiwa ni vigumu kuona wanyama pamoja na ndege kwa karibu kutokana na kutawanyika kwao, ila hii ni tofauti uwapo katika miteremko ya Mlima Meru kwani unaweza kuona vyote kwa pamoja kwa urahisi huku ukiwa unapanda kuelekea kileleni au kushuka.  Unaweza kuona viumbe kama Nyati, Twiga, Nyani, Tembo pamoja na fisi kwa uchache. Kwa wageni wenye bahati wanaweza hata kuwa na nafasi ya kuona chui wakiwa kwenye vivuli au wakiwa wanaondoka taratibu na kupotelea machakani wakiepuka kuonekana na viumbe wengine kama binadamu.
Utalii unaofanyika hapa ni Utalii wa upandaji Milima, utalii wa ekolojia, pamoja na utalii wa kuvinjari nyikani.

MESERANI SNAKE PARK



Hifadhi ya nyoka ya Meserani inayopatikana Arusha ni hazina maalum, kwa wageni na wenyeji kwa madhumuni ya kujiburudisha na kustareheka yenye mazingira ya utulivu. Hifadhi hii ya nyoka iko 25km Magharibi mwa Arusha kando kando ya barabara kuu ilelekeayo katika mbuga maarufu duniani za Serengeti na Ngorongoro.
Ukiwa katika Hifadhi ya nyoka ya Meserani unaweza kufanya shughuli mbalimbali, ikiwemo pamoja na kufanya ziara ya kuongozwa na kujifunza kuhusu baadhi ya nyoka hatari zaidi duniani, kama vile Black na Green Mamba, Egyptian Cobra, Kifutu (Puff Adders) na wengine wengi zaidi. Unaweza kupata nafasi yako ya kupiga picha na kumshika nyoka halisi anayeishi pamoja na kushuhudia Mamba wenye urefu zaidi ya mita 3 na kuendelea, huku ukipata picha yako ya kumbukumbu na kitoto cha mamba.
Pia unaweza kufurahia kwa kujifunza tamaduni mbalimbali za kabila la Kimasaai kwa kutembelea Makumbusho zao pamoja na kupanda Ngamia huku ukizunguka na kufanya safari katika kijiji kilichopo karibu na eneo hili la Meserani.
Pia unaweza kufanya ziara katika kituo cha elimu ambapo Wamasai wanapata nafasi ya kujifunza jinsi ya kusoma na kuandika pamoja na kujifunza tamaduni zao mbalimbali.
Utalii unaofanyika hapa ni pamoja na utalii wa kitamaduni, utalii wa kihistoria juu ya makabila ya kimasai pamoja na nyoka hatari zaidi duniani wapatikanao katika eneo hili.

ARUSHA NATIONAL PARK



Hifadhi ya taifa ya Arusha yenye ukubwa wa kilometa za amraba 328.4, iko umbali wa kilometer 62 kutoka Arusha mjini. Hifadhi hii ina maeneo matatu muhimu ambayo ni; bonde la ngurudoto (Ngurudoto crater) maziwa ya momella ambayo kila moja hotoa mandhari tofauti pamoja na Mlima Meru wenye urefu wa mita 4,566 hali ambayo inaifnya hifadhi hii kuwa na mazingira ya baridi na ya kuvutia.
Viumbe mbalimbali hutumia hifadhii hii kama makazi yao muhimu, baadhi ya viumbe hao ni kama mbega weusi na weupe. Wanyama wengine wanaopatikana kwa wingi katika hifadhi hii ni pamoja a pundamilia, nyati, tembo na digidigi. Aidha unaweza kuwaona chui wakiwa kwenye vivuli vya miti pamoja na makundi kadhaa ya bata maji wakitafuta malisho katika maziwa ya momella. Vilevile hifadhii ni imethibitika inatunza zaidi ya aina 400 za ndege wa aina mbalimbali.
Aina za utalii zinazofanyika katika hifadhi hi ni pamoja na Utalii wa mbuga na kuvinjari nyikanii, Utalii wa majini katika Maziwa ya Momella, utalii wa kupanda Mlima hususani Milima Meru, Utalii wa ekilojia (ecological tourism) pamoja na Utalii wa kupiga picha.

HIFADHI YA TAIFA YA ZIWA MANYARA



Hifadhi ya Taifa ya Ziwa Manyara ni kovutio kingine kinacho lipamba Jiji la Arusha na kuzidi kukamilisha sifa yake ya kuwa kitovu cha ualii Nchini. Hifadhi ya Ziwa Mnayara ni maarufu sana nchini kwa samba wapandao miti. Hifadhi hii inapatika ndani ya Bonde la ufa ambalo kingo zake zinaongeza mandhari nzuri katika Hifadhi hii. Wageni kutoka ndani na nje ya Nchi huja kutembelea hifadhi hii na kujionea maajabu ya dunia haswa viumbe wa porini (wanyama, mimea na ndege). Wanyama wanaopatika katika hifadhi hii ni pamoja na simba, nyati, tembo, chui, pundamilia na wanyama wengine walao majani na nyama. Hifadhi hii inasifika pia kwaa wingi wa ndege haswa heroe, na mnandi ambao wanaonekana katika makundi makubwa na kufanya eneo hili la kitalii kuwa na zaidi ya aina 400 za ndege.
Vilevile hifadhi hii inatunza chemchem ya maji ya moto ambayo ni moja ya maajabu yapatikanayo katika hifadhi hii na inayovutia wageni wengi. Kwa mamilioni ya miaka, maji hayo yamekuwa yakibubujika kutoka ardhini na huonekana yakitoa mvuke kama maji yanayochemka jikoni.
Aina za utalii zinazofanyika katika Hifadhi hii yaTaifa ni pamoja na Utalii wa mbuga na kuvinjari nyikanii, Utalii wa ekilojia (ecological tourism) pamoja na Utalii wa kupiga picha.

HIFADHI YA TAIFA YA TARANGIRE



Hifadhi ya Taifa ya Tarangire ni maarufu kwa makundi makubwa ya tembo wanaoweza kuonekana katika eneo dogo. Tarangire pia ina mandhari nzuri ya kuvutia yanayotokana na maumbile ya mibuyu inayosadikwa kuwa na umri zaidi ya miaka eflu nne.
Wanyama wanaopatikana ndani ya hifadhi hii ni pamoja na pundamilia, nyumbu, swala, simba nyati, kongoni, chui, duma na wengineo wengi. Pia Hifadhi hii ni maarufu kwa ndege ambayo zaidi ya aina 550 za ndege zimerikodiwa katika eneo hili. Mbali na yote hifadhi hii ni maarufu kwa upatikanaji wa chatu wakubwa walio na uwezo wa kukwea miti. Ni kutokana na umaarufu wa hifadhi hii idadi ya wageni wanaotembelea hifadhi hii imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka.
Mto Tarangire ni mto ambao hutiririsha maji yake kipindi chote cha mwaka, kitu ambacho kimeufanya mto huu kuwa kimblio la wanyama wengi wapatikanao katika hifadhi hii hususani kipindi cha ukame wakati mvua hazinyeshi na kupelekea vijito vingine kukauka. Hii pia hupelekea zoezi la kuona wanyama kuwa rahisi kutokana na kuzingira mto huu kwa ajili ya kunywa maji na mawindo pia hususani kwa wanyama walao nyama kama simba.
Aina za utalii zinazofanyika katika Hifadhi hii ya Taifa ni pamoja na Utalii wa mbuga na kuvinjari nyikanii, Utalii wa ekilojia (ecological tourism) pamoja na Utalii wa kupiga picha.

MAKUMBUSHO YA TAIFA YA VIUMBE HAI YA ARUSHA



Ni moja ya makumbusho zinazopatikana katikati ya jiji la Arusha inayopatikana barabara ya Boma karibu na ukumbi wa kimataifa wa mikutano wa AICC, ofisi za Manispaa pamoja na ofisi za Mkoa Arusha. Makumbusho ipo kwenye Boma iliyojengwa na Wajerumani katika miaka 1900 iliyokuwa ikitumika kama jengo la Utawala na mawasiliano wakatiki wa ukoloni wa Kijerumani wakati huo nchi ikijulikana kama Tanganyika.
Makumbusho ilifunguliwa rasmi mnamo mwaka 1987 na kuonesha historia ya binadamu wa kale, ikiwepo pamoja na tafiti zilizofanyika katika bonde maarufu la Olduvai (Olduvai Gorge) na alamaza za miguu wa binadamu wa kale za Laetoli (Laetoli footprints). Pia inafanya Maonyesho juu ya entomolojia ambayo huwasilisha baadhi ya wadudu, ndege na wanyama pamoja na umuhimu wao kiuchumi ambacho pia ni kivutio kikubwa kwa wageni wanaotembelea makumbusho hii.

MAKUMBUSHO YA AZIMIO LA ARUSHA


Makumbusho ya Azimio la Arusha iko katika eneo la Kaloleni katika Jiji la Arusha. Ni ya kwanza kabisa kati ya makumbusho zilianzishwa katika mkoa wa Arusha na mzunguko wa kiutalii wa kaskazini mwa Tanzania. Makumbusho hii ipo katika jengo la kihistoria ambalo mpaka mwaka 1967 lilitumika kama jengo la ustawi wa jamii na ukumbi kwa ajili ya watu wa eneo la Kaloleni. Makumbusho hii ilipata kufunguliwa kwa umma mnamo mwaka 1977 na hasa ilionesha historia ya kisiasa ya Taifa letu. Baada ya kutembelea makumbusho hii utaona picha ya uundaji wa sera ya kujitegemea, mapambano kwa ajili ya uhuru, historia ya Ukoloni, na maendeleo ya kisiasa ya Tanzania.

UKUMBI WA KIMATAIFA WA MIKUTANO WA ARUSHA (AICC)



Ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Arusha (AICC) ulianzishwa tarehe 25 Agosti 1978. Uwepo wa ukumbi huu unafanya Jiji la Arusha kuongeza idadi zaidi za aina za Utalii zinazofanyika katika Jiji hili ukiwemo Utalii wa Mikutano. Ukumbi huu ni mkubwa na umekuwa ukifanya mikutano mbalimbali ya kiserikali na taasisi binafsi kutoka ndani na nje ya nchi. AICC unabaki kama ukumbi na alama muhimu ya utalii katika Jiji la Arusha.

OLDONYO LENGAI



Oldoinyo Lengai yenye maana ya “Mlima wa Mungu” katika lugha ya Kimasai wenye urefu wa Mita 2962 juu ya usawa wa bahari, na ndio Mlima pekee wenye volkano hai unaopatikana Tanzania. Kumbukumbu ya milipuko mkubwa zaidi wa Milima Oldonyo Lengai ulitokea mnamo mwaka 1883, ambao ulirusha majivu yake kwa umbali wa kilomita 100 Kaskazini Magharibi kwa upande wa Loliondo katika mipaka ya Kenya. Kabila maarufu la Kimasai hutumia Mlima huu kwa kufanya ibada zao za kimila wakiupa sifa za Uungu kwa ajili ya kutatua matatizo yao ya kijamii yanayo wakumba kila siku kama ukame na magonjwa.
Utalii uanofanyaika hapa ni utalii wa kupanda milima.

LAKE EYASI



Ni ziwa lenye maji ya chumvi linalopatikana kati ya genge la bonde la ufa na na Milima ya Kidero. Maeneo yazungukayo ziwa Eyasi ni makazi ya kabila maarufu la Wahadzabe ambao ni moja ya makabila machae ya wawindaji yaliyobaki katika bara la Afrika. Wahadzabe wamekuwa wakiishi katika misitu ya acacia na vichaka vinavozunguka maeneo ya ziwa Eyasi kwa atakribani zaidi ya miaka 10,000 iliyopita.
Utalii unaofnyika katika eneo hili ni utalii wa kitamaduni,

ZIWA NATRON



Maeneo yanayozunguka Ziwa Natron yana baadhi ya mazingira ya kushangaza zaidi barani Afrika. Mazingira hayo ni pamaoja na mchanganyiko wa maeneo mpana ya wazi na tambarare, miinuko, Mlima mkubwa wa volkano pamoja na ziwa lenyewe lenye asili ya madini soda yenye rangi mbalimbali, ni dhahiri kwamba eneo hili ni la kuvutia na kupendeza.
Umuhimu wa ziwa hili katika ukanda wa Afrika Mashariki unatokana n ukweli kwamba ndio sehemu pekee katika ukanda huu ambapo panatoa fursa ya ndenge aina ya flamingo kuzaliana kwa wingi.

ENGARUKA


Engaruka inapatikana kilometa 63 kaskazini mwa Mto wa mbu katika barabara ya Oldnyo lengai na ziwa Natron chini kidogo ya genge (escapment) la bonde la ufa. Ni sehemu muhimu ya kihistoria kama inavosemekana miaka 500 iliyopita jamii ya wakulima ya watu elfu kadhaa waliamua kuendeleza kilimo cha umwagiliaji katiaka eneo hili, ila, kwa sababu zisizo julikana wakulima hao waliondoka Engaruka miaka 1700 iliyopita na kuacha magofu ambayo mpaka sasa yanaongelea ni jinsi gani sehemu hii iliendelea kwa kufanya kilimo cha kisasa kwa ajili ya uchumi wao na chakula.
Utalii unaofanyika katika eneo la Engaruka ni utalii wa Kihistoria, na kitamaduni juu ya jamii ya wakulima iliyopata kuishi katika eneo hili miaka 1700 iliyopita.

ZIWA DULUTI



Ziwa Duluti ni ziwa dogo lenye asili ya kivolkano (crater lake) ambalo ni kivutio kingine kinachopatika katika Jiji la Arusha nje kidogo ya Jiji katika mji mdogo wa Tengeru likiwa limezungukwa na msitu mzuri wa asili penye mazingira tulivu penginre kuliko sehemu yeyote ile uliopata kuwa. Ziwa lipo katikati ya msitu mnene wenye mimea mbalimbali ya mwituni pamoja na viumbe hai vingine vikiwemo ndege kama vile Kingfisher, Buzzard, Mnandi, Njiwa, na Barbet na wanyama mbalimbali. Eneo hili linatoa shughuli mbalimbali za kitalii kama vile michezo ya uvuvi, kupanda mtumbwi, matembezi ya mwituni kwa ajili ya kuangalia ndege wazuri wapatikao katika msitu wa ziwa Duluti.
Utalii unaofanyika Ziwa Duluti ni pamoja na utalii wa kwenye maji, utalii wa ekolojia (eco tourism), utalii wa matembezi nyikani.

NGORONGORO CRATER


Ukitokea barabara ya Manyara kuelekea Ngorongoro utapanda mlima mkali uliopo kwenye kuta za bonde la ufa na usifanye kosa la kuacha kutazama mandhari nzuri ya bonde la ufa ufikapo juu. Baada ya hapo utapita katika plateu ya mbulu penye barabara za mianda ambayo ni maarufu kwa kilimo kinachofanywa na watu wa mbulu maarufu kama wairaq. Mbele kabisa kuna msitu mnene uliopo kwenye muinuko mkali ambao ni upande mmoja wa Ngorongoro crater, ambapo pengine hujulikana kama kimbilio maarufu zaidi la wanyama pori duniani. Ukiwa juu ya mzunguko wa creter kwa urefu upatao mita 2400 (futi 8000) na uangaliapo chini utaona sehemu kubwa enye nyasi, misitu pamoja ziwa.
Ngorongoro crater ni moja ya maajabu ya asili ya dunia sehemu inayojulikana zaidi kwa wingi wake wa viumbe hai mbalimbali vya porini na ndio sababu pekee ambayo sehemu hii imekuwa ikiiwavutia wageni wengi kutoka ndani na nje ya nchi. Ingawa Ngorongoro crater in sehemu ndogo ya Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro ambayo inatoa fursa ya kushuhudia aina tofauti za vivutio vya kitalii kwa wageni wake.
Upekee wa Ngorongoro hutokana na ukweli kwamba, inachanganya historia ya wanadamu na muingiliano wa mazingira yake hususani wanyama pori katika eneo moja bila kuathiriana, kitu ambacho kimekuwa ni kigumu kwa sehemu nyingi Afrika na dunia pia.
Aina za utalii zinazofanyika hapa ni pamoja na Utalii wa mbuga na kuvinjari nyikani, Utalii wa ekilojia (ecological tourism), utalii wa kitamaduni na historia, pamoja na Utalii wa kupiga picha.

OLDUVAI GORGE



Katika kipindi cha miaka thelathini iliyopita, imekuwa wazi kuwa pengine Bara la Afika ndilo chimbuko la mwanadamu. Kutoka katika Bara hili ndipo walipoanza kuenea na kutawanyika na kujaza maeneo mengine duniani. Hii ni kutokana na tafiti zilifanywa na kupatikana kwa mabaki ya binadamu wa kale katika eneo la Bonde la Olduvai (Olduvai Gorge) katika Mkoa wa Arusha.
Bonde la Oldupai (mwanzo likitamkwa kama Olduvai) ni eneo maarufu zaidi la Kiakiologijia lipatikanalo Afrika ya Mashariki ambalo limekuwa kivutio muhimu kwa watilii wengi wajao ukandaa huu wa Afrika ya Mashariki hususani pindi wajapo Ngorongoro au wakiwa wanaelekea katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti. Pia ni sehemu muhimu ya kujifunza juu ya historia ya mwanadamu wa kale kwa watalii wa ndani watokao sehemu mballimbali ya nchi.

Tupo tayari kuwajulisha juu ya uzuri wa nchi yetu ya Tanzania, na kuvitangaza vivutio vyote vya utalii vinavopatikana hapa nchini. Kaa tayari kupokea na kuvijua vivutio vingine vipatikanavyo katika Mkoa mwingine wa Tanzania hivi karibuni. 

Kama ilivYo ada, kaulimbiu yetu siku zote ni "UTALII KWA WOTE"



Pages